Blog Post

Wananchi Ruangwa wapongeza ujenzi wa Barabara

 Na Mwandishi Wetu, Lindi

WANANACHI wa eneo la  Nandagala lililopo Wilaya ya Ruangwa Mkoa wa Lindi wamepongeza  hatua ya Serikali ya kujenga barabara ya Ruangwa hadi Nangaga yenye urefu wa km 53.5 inayolenga kusaidia  katika usafiri na usafirishaji wa bidhaa na mizigo  kwenda maeneo mbalimbali nje ya mkoa huo.

Bi. Sofia Juma amesema kuwa kabla ya ujenzi wa barabara hiyo hali ilikuwa mbaya na kusafiri kwenda Mtwara au Dar es salaam iliwalazimu kutumia muda mwingi zaidi kwasababu ya mashimo yaliyokuwepo barabara.

" Kwa sasa barabara hii inaendelea kujengwa na tunapongeza kwa hatua hii  iliyofikia sasa hivi kwenda Dar es salaam  hatutumii muda mwingi  kama mwanzo", amesema  Bi Sofia.

Vilevile, Bi. Fatma Abdallah ameeleza kuwa awali kutumia barabara hiyo hasa wakati wa mvua ilikuwa shida zaidi na magari yaliharibikia njiani.

"Hata nauli imekua nafuu, kutoka shilingi 4500 hadi sasa shilingi 3000. Pia, kusafirisha mazao mfano korosho, ufuta na mbaazi imekua rahisi", ameeleza Fatma.

Ametaja manufaa mengi ya barabara hiyo "Hata mimi binafsi nimepata ajira ya kupika chakula kwa wahandisi wanaojenga hapa na kwa kweli napata fedha za kuhudumia familia yangu".

Aidha, Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan, ameweka jiwe la msingi katika barabara hiyo ya Ruangwa - Nangaga ambayo ni kati ya miradi anayotembelea mkoani humo.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa, Waziri wa Ujenzi Mhe. Innocent Bashungwa pamoja na Viongozi wengine wakati akivuta kitambaa kuweka jiwe la Msingi Ujenzi wa barabara ya Nanganga-Ruangwa-Nachingwea sehemu ya Nanganga -Ruangwa km 53.2. Hafla ya uwekaji wa jiwe hilo la Msingi imefanyika katika Kijiji cha Nanganga Mkoani Lindi tarehe 18 Septemba, 2023.



Post a Comment

0 Comments

Close Menu