Afisa Uhusiano NACTVET Casiana Mwanyika akizungumza na wanafunzi wa shule za Sekondari za Mkoa wa Mwanza kuhusiana na majukumu NACTVET.
BARAZA la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) kupitia ofisi yake ya Kanda ya Ziwa linaelimisha wanafunzi juu ya taratibu za kufanya maombi ya kujiunga na vyuo vya elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi nchini.
Wanafunzi katika shule za sekondari Jijini Mwanza na Manispaa ya Ilemela, wamefikiwa kuanzia tarehe 25 Agosti ambapo zoezi hilo litadumu mpaka tarehe 3 Septemba, 2023.
Mkuu wa Kanda ya Ziwa wa Baraza hilo Bw. Godfrey Muhangwa amesema lengo la kutoa elimu hiyo ni kuwajengea uelewa wanafunzi hao juu ya majukumu ya NACTVET na kuwaelewesha kuhusu taratibu mbalimbali za kufanya maombi ya kujiunga na vyuo vya elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi.
Ziara hiyo mkoani Mwanza imehusisha takribani shule 20 kiwemo za serikali, binafsi na zile zinazomilikiwa na taasisi za kidini. Miongoni mwa shule hizo ni pamoja na Shule ya Sekondari ya Wavulana Bwiru , Sekondari ya Wasichana Bwiru, Musabe , Pamba, Mwanza, Bidii, Omega, Butimba, Baptist, Bujigwa na shule ya wasichana ya Mt. Joseph.
Kwa upande wao, wanafunzi wameushukuru Uongozi wa NACTVET na watumishi wake kwa kuona umuhimu wa kuwajengea uelewa wa taratibu za udahili na mambo muhimu yahusuyo Elmu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi.
NACTVET kanda ya ziwa ni miongoni mwa kanda 7 za Baraza, zilizoanzishwa kwa lengo la kusogeza huduma karibu na wateja wake.
Kanda hiyo inahudumia mikoa 5 ambayo ni Mwanza, Mara, Kagera, Geita na Simiyu na jumla ya Vyuo 78 na vyuo 103 vya ufundi stadi (VETA).
Ziara za kuwaelimisha wanafunzi wa sekondari ni endelevu ambapo shabaha kubwa ni kuwapa uelewa juu ya kazi za Baraza, masuala ya udahili na programu mbalimbali zitolewazo na vyuo vya Kati na vile vya ufundi Stadi.
0 Comments