TABORA
Na Omary Mbaraka
Kambi ya Madaktari Bingwa na Bobezi wa Mhe. Rais Samia imefanikiwa kuanzisha huduma za upasuaji katika Hospitali ya Wilaya ya Sikonge mkoani Tabora, huduma ambayo haikuwepo hapo awali katika hospitali hiyo.
Akizungumza Hospitalini hapo Mganga Mfawidhi wa Hospitali hiyo Dk. Catherine Katisho amesema ujio wa Madaktari Bingwa imekuwa ni neema kwao kwani rufani ambazo zilihitaji upasuaji sasa zitakuwa zikifanyika katika hospitali yao.
"Kwa Mwezi tulikuwa na wastani wa wagonjwa kati ya 25 hadi 30 waliokuwa wakihitaji huduma ya upasuaji hivyo tulikuwa tunalazimika kuwapa rufani kwenda Hospitali ya mkoa Kitete iliyopo umbali wa takribani kilomita 90", amesema Dk. Katisho.
Katisho ameongeza kuwa miundombinu mingi iliyopo hospitalini hapo ilishindwa kutumika kutokana na kutokuwa na utaalamu wa kutosha na ujuzi lakini ujio wa kambi hiyo utawasadia watumishi wao kujifunza namna ya kuitumia.
"Watumishi wetu tumewashikiza kwa kila Daktari Bingwa ili wavune ujuzi kwa Mabingwa hawa na wakiondoka wawe wametuachia maarifa", amefafanua Dkt. Katisho
Madaktari Bingwa wa Rais Samia Suluhu Hassan walikuwa mkoani humo kwa muda wa siku sita kutoa huduma za kibingwa kuanzia Oktoba 07 hadi 13, 2024.
0 Comments