Blog Post

Serikali yahimiza Wananchi kutembelea maadhimisho Wiki ya Elimu

Na Casiana Mwanyika

NAIBU Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia Dkt. Franklin Rwezimula ametoa wito kwa wananchi kutembelea mabanda ya taasisi mbalimbali za Elimu na binafsi zinazoshiriki Maadhimisho ya Wiki ya Elimu Kitaifa, mkoani Pwani ili kupata elimu na uelewa utakaosaidia maboresho ya Elimu nchini.

Dkt. Rwezimula ameyasema hayo akiwa katika banda  la Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET) Oktoba 11, 2023 ikiwa ni siku ya tatu ya Maadhimisho ya Wiki ya Elimu ya Watu Wazima Kitaifa yanayofanyika viwanja vya Maili moja, Kibahamkoani Pwani.

NACTVET imeshiriki Maadhimisho hayo  ambayo huadhimishwa duniani kote mwezi Septemba kila mwaka ambapo Tanzania mwaka huu inaadhimisha Wiki ya Elimu ya Watu Wazima kuanzia kuanzia Oktoba 9 - 13.

Lengo la Maadhimisho hayo ni kuwajengea uelewa wadau wote wa Elimu  nchini kwa kutilia uzito juu ya nafasi ya Elimu ya Watu Wazima na kwamba inaendana na mazingira ya sasa, ambayo ni tofauti na  zamani ambapo elimu hiyo  iliyojikita zaidi kwenye  Kusoma, Kuandika na Kuhesabu. 

Mwelekeo wa sasa unakazia  kisomo ni  chenye manufaa ( Functional Literacy) kwani watu hufundishwa kusoma, kuandika na kuhesabu kuendana na kazi wanazozifanya ili kuwawezesha kufanya vitu tofauti kutokana na mahitaji ya sasa ya jamii yetu, mathalan;  kujifunza kusoma, kuandika na kuhesabu huku walengwa wakijifunza ujuzi  aina mbalimbali kama vile  kutengeneza  sabuni.

NACTVET wamekuwa  wakishiriki  maonesho hayo kama sehemu ya uelimishaji umma na kusogeza huduma za Baraza hilo karibu zaidi na wateja na wadau mbalimbali.

 Kwa kupitia fursa hiyo wananchi wamepata nafasi ya kutatuliwa changamoto zao na kuelimishwa juu ya Majukumu ya NACTVET.

Baraza hilo ni chombo lilichoundwa kwa sheria ya Bunge sura Na.129 kutekeleza jukumu kubwa la kusimamia ubora katika utoaji wa Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi Nchini.

Post a Comment

0 Comments

Close Menu